TUNA IMANI KUPATA USHINDI

Timu za mpira wa vikapu za Kenya kwa wachezaji wenye umri Chini ya miaka 23 mchezo wa 3×3 zimejawa na imani na ari huku zikijiandaa kwa Kombe lijalo la Dunia la FIBA 3×3 kwa U23 huko Ulaanbaatar, Mongolia.
Timu za wanaume na wanawake, zinazojumuisha wachezaji wanane, makocha wawili, daktari wa timu, na mtaalamu wa fiziotherapi, zimekuwa na bidii kwenye kambi ya mazoezi katika uwanja wa Strathmore jijini Nairobi, na ziko tayari kuwakilisha Kenya katika hatua ya kimataifa.
Kikosi cha wanaume kina wachezaji mahiri kama David Gichohi, Elisha Odhiambo, Jackson Waweru, na Denis Koja.
Kocha wa timu ya wanaume Tonny Ochieng na mwenzake wa upande wa wanawake Eunice Ouma wameelezea imani kuwa timu zote mbili zitang’ara nchini Mongolia.
Mashindano hayo yaliyopangwa kufanyika Septemba 27 hadi Oktoba 1 hayatoi tu jukwaa la kuonyesha uwezo wao bali pia hutumika kama fursa muhimu ya kujikusanyia pointi kwa ajili ya Olimpiki ya 2028.
Imetayarishwa na Nelson Andati