#Football #Sports

BANDARI YOUTH FC MABINGWA WA COAST BINGWA FEST

Bandari Youth FC walitawazwa mabingwa wa Coast Bingwa Fest jana Jumapili baada ya kushinda Simba Apparel 1-0 katika Uwanja wa Mbaraki, Kaunti ya Mombasa.

Bao pekee la ushindi lilifungwa na Yusuf Ali, anayejulikana kwa jina la utani “China,” na kuipa Bandari Youth taji hilo.

Fainali ilianza kwa kasi, ambapo Suleiman Kahema wa Bandari Youth alipiga shuti kali kutoka yadi 20 katika dakika ya pili, lakini kipa wa Simba Apparel, Stephen Ogola, aliokoa kwa ustadi.

Dakika ya 26, Bandari Youth walifungua ukurasa wa mabao baada ya China kumalizia mpango mzuri wa kushirikiana na Hafidh Abdillah na Mohammed Tsuma, akiweka mpira kimiani kwa shuti la chini kwenye kona ya goli..

Kabla ya mapumziko, kipa wa Bandari Youth, Francis Katana, alifanya kazi ya ziada kwa kuzuia shuti la Austin Oduor na kuhakikisha timu yake inaongoza 1-0 hadi kipindi cha kwanza kilipomalizika.

Kipindi cha pili kilishuhudia Simba Apparel wakishambulia kwa nguvu kupitia Peter Mwololo, Charles Lumumba, na Bakari Rama, lakini Bandari Youth walitetea kwa uimara na kusimamia mchezo kwa utulivu.

Licha ya presha kubwa kutoka kwa Simba Apparel, Bandari Youth walidhibiti mchezo, wakibaki bila kupoteza mechi yoyote kwenye mashindano na kutwaa ushindi bila kuruhusu bao kwenye fainali.

Imetayarishwa na Janice Marete

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *