HOMEBOYZ WASHINDWA KUREJEA ‘NYUMBANI’
Klabu ya Kakamega Homeboyz ilipoteza nafasi ya kurejea kileleni mwa jedwali la ligi kuu ya soka KPL kufuatia kichapo cha mabao 2-0 mikononi mwa Mathare United wikendi hii, na kuwapa Gor Mahia nafasi ya kuendelea kuongoza licha yao kukosa kuwa na mechi wikendi hii.
Homeboyz ambao wamecheza mechi 9 kufikia sasa, wana pointi 15 katika nafasi ya 2, pointi moja nyuma ya Gor ambao wamecheza mechi 7, AFC Leopards katika nafasi ya 3 kwa pointi 13 baada ya mechi 8.
Katika matokeo mengine, bingwa mtetezi Police FC alimzima bingwa wa zamani Tusker FC kwa kibano cha mabao 2-1, huku Bandari FC wakiandikisha ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Sofapaka.
Posta Rangers walitoa sare ya bao 1 dhidi ya Mara Sugar huku KCB FC na Bidco United wakiumiza nyasi bila sababu.
Imetayarishwa na Antony Nyongesa
English 












































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































