#Football #Sports

LEOPARDS WAMWAGA MVINYO WA TUSKER FC

Klabu ya AFC Leopards iliimarisha uwindaji wake wa ubingwa wa ligi kuu ya soka nchini, KPL, msimu huu, baada ya kuandikisha ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Tusker FC.

Baada ya kipindi kirefu cha tahadhari kwa timu zote 2 katika uwanja wa Nyayo, Leopards walitoa kucha zao na kuumwaya mvinyo, kupitia kwa Hassan Beja katika dakika ya 81.

Ushindi huo ulihakikisha kuwa Ingwe wanawacharaza Tusker nyumbani na ugenini msimu huu, baada ya kuandisha ushindi wa mabao 4-0 katika mkondo wa kwanza Januari mwaka huu.

Wangali katika nafasi ya pili kwa pointi 49, pointi 7 nyuma ya Gor Mahia walioicharaza Shabana mabao 2-1, huku Tusker wakisalia kwenye nafasi ya 7 na pointi 37.

Katika matokeo mengine, Ulinzi Stars walionja ushindi baada ya kipindi kirefu cha ukame ambacho kimewaweka katika hatari ya kushushwa daraja.

Wanajeshi hao walipata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Nairobi United, ingawa bado haujawaokoa.

Posta Rangers walipata ushindi sawa dhidi ya Kariobangi Sharks, huku mechi kati ya Kakamega dhidi ya Bandari na Murang’a Seal dhidi ya Mathare zikiishia kwenye sare ya bao 1-1.

Imetayarishwa na Antony Nyongesa

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *